|

MCHUNGAJI ALITAKA PENZI BILA KINGA,AFIKISHWA MAHAKANI


                                 Jean Felix Bamana akifikishwa mahakamani chini ya ulinzi mkali.
KESI ya kutorosha wanafunzi inayomkabili Mchungaji wa Kanisa la Tanzania Assemblies Of God (TAG), Jean Felix Bamana, Raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Jumatatu wiki hii ilianza kurindima katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi, Kilimanjaro huku upande wa walalamikaji ukiiambia korti, ‘mchungaji alitaka penzi bila kinga’.
Mchungaji huyo alitiwa mbaroni Machi 13, mwaka huu ndani ya Hoteli ya Grand iliyopo Magomeni, Dar akiwa na wanafunzi wawili, watoto wa familia moja, Artha Swai (17) na Angel Swai (19) ambao alidaiwa kuwatorosha kutoka mjini hapa.
Katika kesi ya msingi, mchungaji huyo alidaiwa kuwadanganya watoto hao kwamba alikuwa akiwafanyia mpango wa kwenda kusoma nje ya nchi lakini badala yake aliwaweka hotelini na kumtaka kimapenzi mmoja wao.
SAA 3:30 ASUBUHI AFIKISHWA MAHAKAMANI
Akiwa chini ya ulinzi mkali wa polisi, Amani lilimshuhudia Mchungaji Bamana ambaye alishindikana kufikishwa mahakamani mara tatu mfululizo kwa visingizio vingi, akipandishwa kizimbani huku akikwepa macho ya umati uliofurika kufuatilia kesi hiyo.
MASHITAKA
Akisoma mashitaka yanayomkabili Mchungaji Bamana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi, mbele ya Hakimu Naomi Mwerinde, mwendesha mashitaka ambaye ni wakili wa serikali, Abdallah Chavula alisema mtuhumiwa huyo anashitakiwa kwa makosa mawili.
Chavula alisema, katika makosa hayo, la msingi ni la kutorosha wanafunzi kinyume na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya sheria namba 6 ya mwaka 2008, ibara ya 4, kifungu cha 5, kifungu kidogo 4 (i)a.
Katika mashitaka hayo, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, mnamo Februari 18, mwaka huu, Angel ambaye kipindi hicho alikuwa ni mwanafunzi wa kidato cha tano katika Shule ya Sekondari ya Mtakatifu Marygorethi ya mkoani hapa, akiwa nyumbani kwao eneo la Masama wilayani Hai, alimuomba mdogo wake, Artha amsindikize mjini Moshi.
Mwendesha mashitaka huyo aliendelea kufafanua mbele ya mahakama hiyo kuwa, wanafunzi hao waliondoka nyumbani bila kutoa taarifa na kwamba walifikia Moshi View Hotel ambako walikutana na mshitakiwa huyo.
Ilidaiwa kortini hapo kuwa wakati watatu hao wakifanya mazungumzo, Artha alimueleza mshitakiwa dhamira yake ya kuendelea na masomo baada ya kumaliza kidato cha nne na mtuhumiwa alimhakikishia kwamba kwa kuwa ni mtu wa kuzuguka kila mahali duniani kote angemsaidia kupata shule nje ya nchi.
Ilielezwa kuwa kama ilivyokuwa kwa mdogo wake, Angel naye alihakikishiwa kufanyiwa utaratibu wa kupata shule nje ya nchi ambapo mshitakiwa alimuahidi kumpeleka Uingereza kusomea masuala ya ubunifu na mitindo.
Mwendesha mashitaka huyo aliiambia  mahakama kuwa majira ya saa tisa alasiri, mshitakiwa aliwapa nauli ya teksi kutoka Moshi kuwarudisha nyumbani Masama na kwa kuwa waliondoka bila kuaga, bibi yao aliwagombeza.
Chavula aliendelea kuiambia mahakama kuwa, katika mawasiliano kati ya watatu hao, Mchungaji Bamana alikuwa akimsisitiza Angel afanye uamuzi mgumu wa kuondoka nyumbani kwao na kumfuata Dar kwa sababu wazazi wake (Angel), watakufa muda wowote, yeye na mdogo wake watapata matatizo kama watakuwa hawawezi kujitegemea.
ZAWADI YA SIMU
Mahakama iliendelea kuelezwa kuwa siku ya kwanza kukutana, mshitakiwa alimpa Artha simu ya Samsung Touch Screen na kwamba siku iliyofuata, mtuhumiwa alimpigia simu Angel kupitia simu aliyompa Artha na kuwataka waende mjini wakale naye bata.
Angel na mdogo wake walitoroka nyumbani kwa kutumia usafiri wa teksi ya mtu aliyefahamika kwa jina moja la Yusuf ambapo baada ya kufika mjini walikutana na mchungaji huyo aambaye aliwapeleka Nakumatt Supermarket alipowanunulia biskuti na headphone za simu.
SMS ZA MAPENZI
Mahakama ilielezwa kuwa, pande zote ziliendelea kupigiana simu na kutumiana ujumbe mfupi (SMS) na katika mazungumzo, mshitakiwa aliendelea kuwasisitiza Angel na Artha kutoroka nyumbani na kuongeza kuwa siku iliyofuata mshitakiwa aliondoka kurejea Dar.
ARTHA AMFUATA MCHUNGAJI DAR
Hakimu Mwerinde aliambiwa kuwa, Februari 18, mwaka huu, Artha alimuaga baba yake kuwa anakwenda Machame kumsalimia bibi yake lakini badala yake alikwenda Moshi kukata tiketi ya basi la saa sita linalokwenda Dar.
Majira ya Saa 7:00 mchana, Artha  alimpigia simu Angel kumfahamisha juu ya safari yake na baadaye akawasiliana na mshitakiwa na kwamba mtuhumiwa alimuagiza akifika Ubungo achukue teksi hadi Grand Hotel ya Magomeni.
Baada ya kufika hotelini hapo, Artha alipokelewa na mshitakiwa na kwa pamoja waliingia mapokezi ambapo mtuhumiwa huyo alilipia gharama zote za malazi ya kijana huyo huku akimhakikishia kufuatilia taratibu za kupata hati ya kusafiria siku inayofuata.
ANGEL NAYE ATIMKIA DAR
Mwendesha Mashitaka Chavula aliendelea kuieleza mahakama kuwa, siku mbili baada ya Artha kufika Dar, Februari 20, Angel alitumiwa shilingi laki moja kwa mtandao kupitia simu ya dereva teksi.
Katika fedha hizo, Sh. 40,000 alitumia kama nauli ya teksi kumtoa Masama hadi Moshi Mjini na zilizosalia, Sh. 60,000 zilitumika kwa nauli ya kwenda Dar.
Chavula alidai kuwa Angel alitumia Sh. 18,000 kukata tiketi ya basi na kwamba mara tu baada ya kufika Dar, alipokelewa na mshitakiwa huyo katika Hoteli ya Grand
MCHUNGAJI ATAKA PENZI BILA KINGA
Katika jambo lililoshtua wengi mahakamani hapo ni pale mwendesha mashitaka huyo alipoiambia korti kuwa mshitakiwa alitaka penzi kwa Angel.
Alisema kuwa katika harakati za kufanikisha azma yake ya kufanya mapenzi na Angel, mchungaji Bamana alikuwa akishinda kutwa katika chumba cha msichana huyo.
Ilidaiwa kuwa mchungaji huyo alikuwa akimshawishi Angel kwa njia zote kufanya naye mapenzi bila kinga!
Mwendesha mashitaka huyo alisema kuwa mara zote, Angel alikataa na kumshauri mchungaji kuwa kama anataka kufanya naye mchezo huo mchafu basi atumie kinga, kitu ambacho mchungaji huyo hakuwa tayari kukifanya.
Ilielezwa kuwa baada ya kugonga mwamba kupata penzi, mchungaji aliambulia kumshikashika na kumbusu mara kwa mara, kitendo kilichomfanya mdogo wake Angel, Artha aanze kuingiwa na shaka pamoja na kwamba walikuwa wakitarajia kusaidiwa.
MCHUNGAJI AKANA MASHITAKA
Upande wa mshitakiwa ulipotakiwa kuwasilisha utetezi wa mashitaka yote mawili, mshitakiwa akiongozwa na mawakili wawili, Erick Gabriel na Rongino Myovela pamoja na kukubaliana na maelezo lakini walikana mashitaka yote.
MASHAHIDI
Kutokana na ugumu wa shitaka hilo, mwendesha mashitaka baada ya kushauriana na mawakili wa mchungaji, aliiomba mahakama iahirishe zoezi la kusikilizwa kwa kesi hadi pale upande wa mshitakiwa utakapopeleka mashahidi nane na vielelezo.
Baada ya kujiridhisha na maelezo ya upande wa mashitaka na kukubaliana na ombi la mwendesha mashitaka, Hakimu Mwerinde aliahirisha kesi hiyo hadi Juni 3, mwaka huu itakaposikilizwa tena.
chanzo:.globalpublishers

Posted by Unknown on 6:37 AM. Filed under , , . You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0. Feel free to leave a response

0 comments for "MCHUNGAJI ALITAKA PENZI BILA KINGA,AFIKISHWA MAHAKANI"

Leave a reply